1. Ada
  2. Magonjwa
  3. Vidonda vya kinywani

Vidonda vya kinywani

Imeandikwa na Timu ya Ada ya Maarifa ya Kitiba

Imesasishwa tarehe

Vidonda vya kinywani ni nini?

Vidonda vya kinywani (aphthous ulcers) ni kati ya vidonda mbalimbali vinavyotokea kwenye utando ute (mucous membranes), kawaida ndani ya mdomo (kinywani). Majina mengine ya vidonda vya kinywani hujumuisha aphthous stomatitis na vidonda vya canker. 1

Vidonda vya kinywani kawaida vina umbo la mviringo na hutokea sehemu laini kinywani kama vile, upande wa ndani wa midomo, mashavu au chini ya ulimi. Vidonda hivi sio vya saratani, haviambukizwi na huweza kutokea kama kidonda kimoja au vikundi. Mara nyingi, vidonda vya kinywani hujirudia - hali inayojulikana kama vidonda vya kinywani vinavyojirudia (recurrent aphthous stomatitis au RAS)- ambapo kila kipindi hudumu kwa siku 7 hadi 10. 2 Kesi hizi hutokea mara chache sana, na ni nadra sana kuvimba tezi za limfu kama dalili ya kwanza ya vidonda vya kinywani.

Sababu ya ugonjwa huu kutokea haijulikani, na hamna tiba, lakini kuna machaguo ya matibabu ya kutibu maumivu yanayoweza kusababishwa na vidonda.

Vizuri kujua: Vidonda vya kinywani ni aina kuu ya vidonda kwenye mdomo, lakini sio aina pekee ya vidonda.

Kuna aina kuu tatu: 3

Vidonda vidogo vya kinywani (Minor aphthous ulcers)

Hivi hutokea sana. Ni vidogo- kawaida chini ya 5mm kwa upana- na huweza kutokea kama kidonda kimoja au mkusanyiko wa vidonda. Kwa kawaida havisababishi maumivu sana.

Vidonda vikubwa vya kinywani (Major aphthous ulcers)

Hivi hutokea mara chache zaidi, kawaida ni 5mm au zaidi kwa ukubwa na hutokea aidha moja pekee au viwili kwa pamoja. Vinaweza kusababisha maumivu, haswa wakati wa kula au kunywa, na huweza kudumu kwa muda wa wiki mbili hadi miezi kadhaa.

Vidonda vya herpetiform (Herpetiform ulcers)

Hivi hutokea kukiwa na vidonda vidogovidogo vingi vinavyoungana na kutengeneza kidonda kikubwa kisichokuwa na umbo la kawaida. Vidonda vya herpetiform huitwa hivyo kwa kuwa vinafanana kwa muonekano na hepesi (herpes), hata hivyo vidonda vya herpetiform havisababishwi na virusi vya hepesi simplex.

Dalili za vidonda vya kinywani

Licha ya vidonda vyenyewe, ugonjwa huu una dalili chache sana. Kabla ya vidonda kutokea, baadhi ya watu huweza kupata hisia ya kama kuungua au kuwashwa ndani ya kinywa, ambayo inaweza kusababisha. Punde tu vidonda vinapotokea, viwango tofauti vya maumivu katika eneo husika mara nyingi hutokea.

Vidonda vya kinywani hufananaje?

Vidonda vya kinywani kawaida vina kina kifupi na vyenye rangi ya njano ambayo haijakolea mwanzoni, na hubadilika kuwa rangi ya kijivu kadri ugonjwa unavyoendelea. Vinaweza kuwa na mviringo mwekundu pembeni au kuonekana vyekundu kabisa ikiwa kuna inflamesheni (sehemu ya mwili kuvimba, kuwa nyekundu, yenye joto na maumivu). Kulingana na eneo ambalo vidonda vipo, inaweza kuwa shida kula, kunywa na kuongea.

Vizuri kujua: Hali inapokuwa mbaya zaidi, vidonda vya kinywani huweza kusababisha kuvimba kwa tezi za limfu, homa na uchovu. 4

Vyanzo vya vidonda vya kinywani

Chanzo au vyanzo halisi vya vidonda kinywani havijulikani. Hata hivyo kuna uwezekano kichochezi kimoja au mchanganyiko wa vichochezi nje ya mwili huweza kusababisha hali hii. Maumbile pia huweza kuchangia, kwani asilimia 40 ya watu wenye vidonda wana historia ya ugonjwa huu katika familia. Vidonda vya kinywani huathiri takribani mtu mmoja kati ya watu watano na mara nyingi hutokea kwenye umri kati ya miaka 10 na 19.

Vichochezi vya vidonda vya kinywani vinavyowezekana ni pamoja na: 5

  • Msongo wa kihisia
  • Jeraha dogo ndani ya kinywa, kwa mfano kutokana na kukatwa, kuungua au kujing’ata wakati wa kula, matibabu ya meno, kupiga mswaki kwa nguvu au meno bandia yasiyotosha vizuri
  • Historia ya ugonjwa huu kaitka familia
  • Sodium lauryl sulfate – dutu inayopatikana kwenye baadhi ya dawa za mswaki na dawa za kusukutua; dutu hii haijathibitishwa kuchochea hali hii kutokea, lakini inajulikana kuongeza muda unaohitajika kwa vidonda kupona
  • Vyakula na vinywaji fulani, ikiwa ni pamoja na kahawa, chokoleti, mayai na jibini (cheese), pamoja na vyakula vyenye asidi au pilipili
  • Upungufu wa vitamini pamoja na/au madini fulani ikiwa ni pamoja na zinki, B-12, folate na madini ya chuma
  • Mzio wa bateria waliopo kinywani
  • Matumizi, pamoja na kuacha, matumizi ya bidhaa za tumbaku
  • Mabadiliko ya homoni kutokana na ujauzito
  • Kuwa na udhaifu wa mfumo wa kinga, kutokana na magonjwa fulani ya muda mrefu (Upungufu wa kinga)

Msongo (Stress) ni kisababishi kikuu cha vidonda vya kinywani. Ingawa msongo hausababishi vidonda vya kinywani moja kwa moja, unaongeza uwezekano wa kuvipata na unaweza kuathiri mchakato wa vidonda kupona. 6 7 Vidonda vya kinywani vinaweza kusababisha msongo kwa kuathiri jinsi na ni vitu gani aliyeathirika anaweza kula na kunywa.

Vizuri kujua: Madaktari wa meno wanaweza kutoa ushauri wa mbinu za kupunguza hatari ya kupata vidonda vya kinywani, kwa mfano kupendekeza dawa za mswaki na za kusukutua zisizokuwa na sodium lauryl sulfate au kutoa ushauri wa vifaa na njia sahihi vya kupiga mswaki ili kupunguza uwezekano wa kupata jeraha kinywani.

Baadhi za dawa zinahusishwa na upataji wa vidonda, hata hivyo, sio kila wakati zinasababisha vidonda vya kinywani. Hizi hujumuisha: ref8 ref9

  • Nicorandil, dawa inayotumika kutibu Chembe ya moyo (angina pectoris), ambao ni ugonjwa wa moyo
  • Ibuprofen na dawa nyingine zinazotumika dhidi ya inflamesheni
  • Tiba ya nikotini Oral nicotine replacement therapy opposed to patch replacement therapy
  • Dawa kama vile aspirini ikiwa zimeachiwa kuyeyuka mdomoni badala ya kumezwa
  • Madawa ya kulevya kama vile kokeini

Mara chache sana, vidonda vinavyojirudia inaweza kuwa dalili ya ugonjwa mbaya zaidi, ikiwa ni pamoja na:

  • Ugonjwa wa Crohn
  • Ugonjwa wa siliaki
  • Ugonjwa wa Behcet
  • VVU/UKIMWI

Vidonda ambavyo havina dalili kwa magonjwa haya, ingawa sio vidonda vya kinywani lakini vinafana sana na vidonda vya kinywani na kwa hivyo vinaitwa vidonda kama vidonda vya kinywani. ref10

Watu wanaopata vidonda vya kujirudia au vidonda ambavyo vinachukua muda kupona, haswa ambavyo vinauma au vinavyoambatana na dalili nyingine wanapaswa kumuona daktari haraka ikiwezekanvyo. Ikiwa wewe au mtu mwingine ana vidonda vya kinywani vinavyojirudia au vidonda visivyopona, unaweza kufanya tathmini ya dalili kwenye app ya Ada wakati wowote.

Utambuzi wa vidonda vya kinywani

Katika visa vingi, haswa ikiwa hali hii haijirudii, utambuzi hufanywa kulingana na uchunguzi wa kimwili na tathmini ya historia ya matibabu ya mtu.

Tathmini na vipimo sahihi kwa vidonda vinavyojirudia ni muhimu kutokana na hali hii kuwa na uhusiano na magonjwa makali kama vile ugonjwa wa siliaki (celiac disease), magonjwa ya inflamesheni kwenye utumbo kama vile ugonjwa wa Crohn, au magonjwa yanayosababisha udhaifu wa mfumo wa kinga, kama vile VVU/UKIMWI. Mchakato wa utambuzi huweza kuhusisha kutofautisha magonjwa haya na vidonda vya kinywani kwa kufanya vipimo vya damu au, mara chache sana, kufanya vipimo vya gastroscopy au colonoscopy (kuanglia ndani ya tumbo au utumbo kwa kutumia kamera), pamoja na kuchukua sampuli za tishu. 8 Mwelekeo wa vipimo vya utambuzi utagemea uchunguzi utakaofanywa na daktari kuhusi ukali wa dalili za mtu na uwepo wa dalili nyingine.

Madhara ya vidonda vya kinywani

Ingawa vidonda vingi vya kinywani huisha ndani ya wiki mbili, mara chache sana vinaweza kupata maambukizi ya bakteria. Hii kawaida hutokea katika hali kali zaidi, ambapo eneo lenye kidonda ni kubwa.

Katika kesi ambazo kuna maambukizi ya bakteria, dawa ya kusukutua yenye antibiotiki na mbinu nyingine za kudhibiti maumivu huweza kupendekezwa. Katika baadhi ya matukio, dawa za antibiotiki za kumeza huweza kuhitajika. (tazama kifungu cha matibabu hapo chini). 8

Matibabu ya vidonda vya kinywani

Hamna tiba ya vidonda vya kinywani au vidonda vya canker, lakini kuna njia ya kudhibiti dalili. Katika matukio mengi, vidonda hupotea bila matibabu na kuepuka kula vyakula vigumu au vinavyokera k.m. mananasi, kuweka vitu vya baridi kwenye eneo lililoathirika na ikihitajika kutumia dutu zinaketa ganzi, kama vile lidoocaine au benzocaine ya kupaka, huwa inatosha kudhibiti maumivu.

Matibabu zaidi yakihitajika, kuna machaguo kadhaa, na chaguo hutegemea maoni ya daktari ya jinsi tiba ipi itafanya kazi kwa ufanisi zaidi, kulingana na eneo na ukubwa na kidonda na afya kwa ujumla ya aliyeathirika. 9

Tiba dhidi ya inflamesheni

Dawa za kupaka dhidi ya inflamesheni zinazopakwa moja kwa moja kwenye eneo lililoathirika huweza kusaidia kupunguza dalili za vidonda vya kinywani, haswa vidonda vidogo. Dawa hizi zinapaswa kupakwa kati ya mara mbili hadi nne kwa siku, tafadhali fuata maelekezo maalum ya mfamasia au daktari wako.

Matibabu ya antiseptiki na Antibiotiki kwaajili ya vidonda vya kinywani

Kutumia dawa ya kusukutua k.m. yenye chlorhexidine, mara mbili kwa siku, au jinsi daktari wako alivyopendekeza huweza kuwa sehemu ya matibabu ya vidonda vya kinywani 10

Mara chache sana daktari anaweza kupendekeza dawa za antiobitiki za kupaka au kumeza, kama vile tetracy line au minocycline, ambazo huweza kusaidia kutibu vidonda. Kawaida hizi hutolewa kama dawa ya kusukutua, ambapo antibiotiki huyeyushwa kwenye maji, na mtu husukutua na kutema. Inaweza kuhitaji kufanya hivi mara kadhaa kwa siku kwa siku kadhaa. 11

Vizuri kujua: Dawa za kusukutua zenye antibiotiki ya tetracycline inapaswa isitumiwe na watoto wenye umri chini ya miaka nane au hata zaidi, kulingana na mapendekezo ya daktari wako, kwa kuwa zinaweza kusababisha meno kubadilika rangi.

Matibabu mengine ya vidonda vya kinywani

Matibabu mengine huweza kujumuisha dawa za steroidi za kupaka, au mara chache sana za kumeza, kwa kawaida zinatumika ikiwa vidonda haviponi licha ya matibabu mengine; naitreti ya fedha (silver nitrate); dawa nyingine za ganzi; na virutubisho (vyenye folate, zinki au vitamini ya B-12, kwa mfano). 12

Tiba za nyumbani za vidonda vya kinywani

Kuna tiba kadhaa maarufu za nyumbani kwaajili ya vidonda vya kinywani, ikijumuisha: 13

  • Kusukutua mdomo na maji yenye chumvi
  • Kusukutua mdomo na maji yaliyochanganywa na magadi (baking soda)
  • Kupaka maziwa ya magnesi kwenye kidonda baada ya kusukutua
  • Kuweka barufu kwenye eneo lililoathirika ili kupunguza kuvimba
  • Dawa za kupaka zenye ganzi zinazotumiwa meno yanapoota ili kudhibiti maumivu na kero
  • Kupunguza msongo (stress)
  • Kuepuka vyakula vigumu au vyakula vinavyoweza kukwaruza sehemu ya ndani ya mdomo

Virutubisho kama vile vidonge vya Vitamini B-12, vitamini D, folate au zinki huweza kupunguza hatari ya kupata vidonda vya kinywani.

Kuzuia kupata vidonda vya kinywani

Ili kupunguza uwezekano wa kupata vidonda, haswa kwa wale wenye historia ya vidonda vya kinywani vinavojirudia, hatua kadhaa huweza kuchukuliwa.

  • Kuepuka kula vyakula vinavyoweza kusababisha vidonda kwa mtu binafsi
  • Kuhakikisha una lishe bora, yenye idadi ya kutosha ya virutubisho ya vitamini
  • Kudumisha usafi mzuri wa kinywa na kutumia mswaki laini ili kuepuka kukera kinywa
  • Kupunguza msongo na kupata uzingizi wa kutosha

Matokeo ya vidonda vya kinywani

Vidonda vya kinywani kwa kawaida sio hatari na huisha vyenyewe bila matibabu maalum.

Vidonda vinavyopona vyenywe ndani ya wiki kadhaa sio ishara ya saratani ya kinywa na haviambukizwi. Vidonda, hata hivyo, huweza kuuma sana na kukera, haswa kama vinajirudia. Watu wengi huona kuwa wanaacha kupata vidonda hivi kadri umri unavyoongezeka.

Vizuri kujua: Ikiwa kidonda au kikundi cha vidonda haviponi ndani ya wiki tatu, au vinadumu kwa zaidi ya wiki tatu, aliyeathirika anapaswa kumuona daktari haraka iwezekanvyo kwa ajili ya vipimo. Katika baadhi ya matukio, kidonda kisichopona huweza kuwa ishara ya saratani ya kinywa.

Maswali Yanayoulizwa Mara kwa Mara (FAQs) kuhusu Vidonda vya kinywani

S: Je kuna tiba za nyumbani za vidonda vya kinywani?
J: Kuna tiba kadhaa maarufu za nyumbani za vidonda vya kinywani, ikijumuisha: 14 15

  • Kusukutua mdomo na maji yenye chumvi
  • Kupaka kiwango kidogo cha maziwa ya magnesi kwenye kidonda baada ya kusukutua
  • Kunyonya barafu ili kupunguza kuvimba
  • Dawa za kupaka zinazoleta ganzi
  • Kuepuka vyakula vigumu au vyakula vinavyoweza kukwaruza sehemu ya ndani ya mdomo au kukera kutokana na vyakula hivyo kuwa na asidi, kwa mfano mananasi, malimau, machungwa au nyanya, wakati kuna kidonda
  • Kupunguza msongo

S: Naweza kupata vidonda vya aphthous kwenye sehemu za siri?
J: Ndio, ingawa vidonda vya aphthous hutokea mara nyingi kinywani, vinaweza pia kutokea kwenye sehemu za siri, Hii ni kawaida zaidi kwa wanawake, ambapo vidonda mara nyingi hutokea kwenye vulva (sehemu ya nje ya uke) au ngozi ya karibu. Vidonda hivi vina muonekano sawa na vidonda vya kinywani na huweza kuuma kama vidonda vya kinywani. 16

S: Ni salama kufanya ngono ya kinywa ikiwa anayefanya tendo hili ana vidonda vya kinywani?
J: Kwa kuwa ngozi ndani ya kinywa imechanika, vidonda vya kinywani huongeza hatari ya kupata magonjwa ya zinaa kama vile hepesi, kisonono, kaswende na klamidia. Hatari hii inaweza kupunguzwa kwa utumiaji wa kondomu na dental damu (kitambaa cha latex kinachotumika kuzuia uwasiliano wa moja kwa moja kati ya kinywa na sehemu za siri). 17 Utunzaji mzuri na mbinu sahihi za usafi wa kinywa huweza kupunguza hatari ya kupata baadhi ya vidonda vya kinywani au kuchanika kwa ngozi kinywani.

S: Je, uvutaji sigara huweza kusababisha vidonda vya kinywani?
J: Uvutaji sigara huweza kufanya vidonda vya kinywani kuwa vibaya zaidi. Nikotini kwenye moshi wa sigara huweza kupunguza idadi ya damu inayofika kwenye mdomo na fizi, ambayo huweza kupunguza kasi ya uponaji wa vidonda vingi kinywani. 18 Uponaji polepole wa vidonda humaanisha kuwa kipindi cha maumivu kinaongezeka na inaongeza hatari ya kupata maambukizi.

Wakati huohuo, inaonekana kuwa uvutaji sigara huweza kupunguza hatari ya kupata vidonda vya kinywani, kwa kuwa inafanya seli ndani ya kinywa kuwa ngumu. 19 Hata hivyo, uvutaji sigara una madhara mengine mengi mwilini na unapaswa kuepuka kuvuta sigara.

S: Vidonda vya kinywani vinavyojirudia (RAS) ni nini?
J: Vidonda ya kinywani vinavyojirudia au kitaalamu recurrent aphthous stomatitis (RAS) ni jina la hali ya kupata vidonda vya kinywani mara kwa mara. Ingawa inawezekana kupata vidonda vya kinywani mara moja, hali hii kujirudia ni kawaida zaidi. 20 Vipindi vya kujirudia kwa vidonda vya kinywani mara nyingi hutokea kila baada ya miezi au siku kadhaa na hudumu kwa siku 7 hadi 10.

S: Kuna uhusiano gani kati ya vidonda vya kinywani na ugonjwa wa Behçet?
J: Ugonjwa wa Behçet husababisha inflamesheni (sehemu ya mwili kuvimba, kuwa nyekundu, yenye joto na maumivu) ya sehemu mbalimbali mwilini. Ugonjwa wa Behçet huchukuliwa kama ugonjwa wa kinga nfasia (autoimmune disease) na baadhi ya wataalamu na wengine husema ni ugonjwa wa inflamesheni unaosababishwa na mfumo wa kinga (autoinflammatory). Magonjwa ya inflamesheni inayosababishwa na mfumo wa kinga, sawa na magonjwa ya kinga nafsia, husababishwa na mfumo wa kinga kufanya kazi kupita kiasi na kushambulia tishu za mwili na hatimaye kusababisha inflamesheni. 21 Dalili moja ya ugonjwa wa Behçet inayotambulika sana ni uwepo wa vidonda vya kinywani, pamoja na vidonda kwenye sehemu nyingine za mwili, ikiwa ni pamoja na sehemu za siri. Pamoja na hayo hii mara nyingi hutokea pamoja na inflamesheni kwenye sehemu ya jicho, hii huitwa uveitis. Ingawa vidonda vya kinywa ni dalili ya ugonjwa wa Behçet, vidonda vya kinywa hutokea sana, na ugonjwa wa Behçet ni ugonjwa adimu. Watu wachache sana wenye vidonda vya kinywani wana ugonjwa wa Behçet. 22

S: Complex aphthosis ni nini?
J: Complex aphthosis ni jina lililopewa hali ya kuwa na vidonda vya kinywani kila wakati au vidonda vya kinywani au sehemu za siri vinavyojirudia bila kuwa na ugonjwa wa Behçet. Ikiwa hali hii inadhaniwa kuwepo, mtu anapaswa kupata msaada wa kiafya kwa ajili ya utambuzi na matibabu. 23

S: Je, ugonjwa wa systemic lupus erythematosus unaweza kusababisha vidonda vya kinywa?
J: Vidonda vya kinywani huwaathiri takribani nusu ya watu wenye ugonjwa wa systemic lupus erythematosus, ugonjwa wa kinga nafsia. Vidonda vyenye uhusiano na Lupus sio sawa na vidonda vya kinywa, na ingawa vinaweza kuuma kwa baadhi ya watu, mara nyingi vidonda hivi haviumi. Mara nyingi vinatokea kwenye sehemu ya juu ya kinywa, lakini vinaweza kutokea kwenye fizi, midomo na upande wa ndani wa mashavu. Vidonda hivi vinafanana na vidonda vya kinywani, kwa kuwa ni vyekundu kwa rangi, lakini vinaweza kutofautiana katika muonekana, k.m. baadhi huweza kuwa na rangi nyeupe. 24 25 Pia watu wenye lupus huweza kupata vidonda puani. 26

S: Je ugonjwa wa ucheuaji asidi (gastroesophageal reflux disease(GERD/GORD) unaweza kusababisha vidonda vya kinywani?
J: Ugonjwa wa ucheuaji asidi (Gastroesophageal reflux disease), pia hutambulika kama ucheuaji asidi, ni hali ambayo asidi kutoka tumboni hurudi nyuma hadi kwenye umio, na mara chache sana, hadi kinywani. Ikiwa asidi inaingia kinywani, GERD inaweza kusababisha mmomonyoko wa enameli ya jino na ladha ya asidi. Vidonda vya kinywani huweza kutokea. GERD pia huweza kusababisha hisia ya koo kuuma, na katika baadhi ya matukio, inflamesheni na vidonda vya koo na umio huweza kutokea. Ikiwa GERD inasababisha vidonda, mara nyingi vitapatikana kwenye sehemu ya nyuma ya kinywa, nyuma ya ulimi na sehemu ya nyuma ya koo, kutokana na njia ambayo asidi hutumia kurudi juu. 27

S: Je, kemotherapi (tiba ya dawa) inaweza kusababisha vidonda vya kinywani?
J: Ndio, kemotherapi (tiba ya dawa) mara nyingi husababisha vidonda vya kinywani. Kemotherapi huweza kusababisha inflamesheni ya utando ute kwenye koo na kinywa, na kusababisha vidonda kinywani. 28 Kwa kawaida, ikiwa vinatokea kinywani, hali ya maumivu na vidonda vinavyosababishwa na kemotherapi hutambulika kitaalamu kama stomatitis na huweza kuhusiana na mucositis, hali inayoathiri eneo kubwa zaidi la utando ute (mucosal lining) wa mfumo wa umeng’enyaji chakula. 29 Kwa taarifa zaidi, soma kuhusu madhara ya kemotherapi.

S: Je, aina C ya Homa ya ini inaweza kusababisha vidonda ya kinywa?
J: Ndio, aina C ya homa ya ini au matibabu yake wakati mwingine huweza kusababisha vidonda vya kinywani au matitizo mengine ya kinywa, kama vile meno kuoza au kinywa kinachoathirika kirahisi k.m. kuathiri uzalishaji wa mate na kusababisha kinywa kikavu. 30 Kwa kuwa homa ya ini aina C ni ugonjwa wenye mambo mengi, watu wenye ugonjwa huu wanapaswa kupata ushauri wa wataalamu wa afya kuhusu wasiwasi wowote walionao na kabla ya kuanza matibabu yoyote.

S: Je, vidonda vya kinywa ni dalili ya saratani?
J: Kidonda cha kinywani kisichopona wakati mwingine ni dalili ya saratani ya kinywa. Hata hivyo, ni idadi ndogo sana ya vidonda vya kinywa ambavyo ni ishara ya saratani. Vidonda vya kinywani venye uhusiano na saratani kawaida hutokea kwenye eneo moja kuliko katika vikundivikundi na hutokea bila sababu yoyote. 31 Ikiwa kidonda kwenye kinywa bado kipo kwa zaidi ya wiki tatu, kina sababisha dalili ambazo mtu anashindwa kumudu kama vile kutoweza kula au kunywa kutokana na maumivu/ au bado kidonda bado kinaendelea kuwepo hata baada ya matibabu, inashauriwa kwa mtu huyu kumuona daktari.

Dalili nyingine za saratani ya kinywa hujumuisha: 32

  • Mabaka meupe au mekundu yanayoenedelea au yasiyopata nafuu kwenye fizi, upande wa ndani wa shavu, findofindo (tonsils)
  • Maumivu ya mdomo yanayoendelea
  • Uvimbe kwenye shavu
  • Maumivu ya koo yanayoendelea
  • Hisia kuwa kuna kitu kimekwama kooni
  • Ugumu wa kumeza, kutafuna, kusogeza taya au ulimi

S: Je, vidonda vya kinywani vinaweza kutokea kwenye fizi?
J: Ndio, vidonda vya kinywani vinaweza kuathiri fizi. Pia ulimi, upande wa ndani wa mashavu na midomo huweza kuathirika.

S: Kuna tofauti gani kati ya vidonda vya homa na vidonda vya kinywani?
J: Vidonda vya homa, pia hujulikani kitaalamu kama “herpes labialis” (cold sores), husababishwa na virusi vya Hepesi simplex aina ya 1 au 2. Vidonda vya kinywani havisababishwi na virusi. Vidonda ya homa kawaida hutokea kwenye pembe za kinywa, midomo, pua na eneo kati ya mdomo wa juu na pua.

Vidonda vya homa vinaweza kuambukiza kirahisi sana. Vidonda vya kinywani kawaida hutokea ndani ya kinywa, na haviathiri pua na haviwezi kuambukiza.