1. Ada
  2. Magonjwa
  3. Ugonjwa wa bawasiri

Ugonjwa wa bawasiri

Imeandikwa na Timu ya Ada ya Maarifa ya Kitiba

Imesasishwa tarehe

Bawasiri ni nini?

Bawasiri ni kuvimba kwa mishipa ya damu iliyopo ndani ya au katika eneo linalozunguka njia ya haja kubwa. Ni hali ambayo inaweza kusababisha nyama kujitokeza nje. Hivyo bawasiri inaweza kuwa bawasiri ya ndani au bawasiri ya nje. Ugonjwa huu unaweza kusababisha mwasho, maumivu na damu au kamasi kutoka wakati wa kujisaidia haja kubwa ingawa wakati mwingine hauna dalili. 1 Madhara ya bawasiri ya ndani ni pamoja na damu kutoka wakati wa kujisaidia, damu kuganda ndani ya mishipa ya damu na maumivu.

Kutokea kwa bawasiri kunaweza kuhusishwa na hali kama uzee, ujauzito, kuharisha au choo kufunga (constipation), saratani kwenye nyonga au kuketi kwa muda mrefu. Tiba ya bawasiri inategemea aina ya bawasiri na ukubwa wa tatizo. Matibabu ya bawasiri yanaweza kuhusisha matumizi ya dawa au upasuaji mdogo.

Dalili za Bawasiri

Inakadiriwa 40% ya watu wenye bawasiri hawana dalili za moja kwa moja. 2 Dalili za bawasiri hujumuisha maumivu, mwasho na hisia ya kitu kinachokera katika eneo linalozunguka njia ya haja kubwa. Baadhi ya watu hupata shida kujisaidia haja kubwa na hutokwa damu wanapojisaidia. Wakati mwingine mishipa ya damu huweza kujitokeza nje. Ikiwa hali hii inatokea, inawezekana kuhisi uvimbe mdogo katika eneo husika.

Vihatarishi vya Bawasiri

Bawasiri hutokea pale shinikizo huongezeka kwenye mishipa ya damu inayozunguka njia ya haja kubwa. Hii huweza kuwa matokeo ya kitu kinachokandamiza utumbo, kama vile wakati wa ujauzito, au huweza kutokea kutokana na kujikamua sana wakati wa haja kubwa kutokana na kufunga choo au kuharisha kwa muda mrefu. Hali hii hutokea sana na hutokea zaidi kadri umri unavyoongezeka. Watu wenye uzito wa kupita kiasi wana uwezekano mkubwa wa kupata bawasiri. Vitu vingine vinavyoongeza hatari ya kupata bawasiri ni pamoja na:

  • Kuwa na uzito wa mwili kupita kiasi, ujauzito, na kula vyakula visivyo na nyuzinyuzi (fibre) za kutosha
  • Kubeba vitu vizito mara kwa mara
  • Kuhara kwa muda mrefu na kufunga choo (constipation)
  • Kujamiiana kinyume na maumbile
  • Historia ya uwepo wa ugonjwa wa bawasiri katika familia
  • Magonjwa yanayoathiri njia ya haja kubwa
  • Kuketi kwa muda mrefu
  • Uzee na matatizo ya kutopata choo. 1

Utambuzi wa Bawasiri

Utambuzi hufanywa na daktari kwa kuchukua maelezo ya mgonjwa na kuchunguza njia ya haja kubwa. Uchunguzi wa njia ya haja kubwa hujumuisha kuangalia eneo hili na kuingiza kidole taratibu kuchunguza sehemu ya ndani ya njia ya haja kubwa. Ikiwa bawasiri hazionekani kirahisi, au sababu ya kutoka damu haijaeleweka vizuri, uchunguzi wa ziada huweza kufanywa ili kuhakikisha hamna sababu nyingine ya dalili hizi.

Matibabu ya Bawasiri

Bawasiri inatibika na kuna njia mbalimbali za kutibu bawasiri. Tiba halisi ya bawasiri ni kuhakikisha kupata choo kilaini na kuepuka kufunga choo, ili kuepuka hali kuwa mbaya zaidi. Krimu za kupaka na dawa za kuingiza katika njia ya haja kubwa (suppositories) zinaweza kusaidia kupunguza uvimbe, mwasho na maumivu. Dawa hizi hupatikana katika maduka ya dawa. Kuna matibabu mengine ambapo sindano au kamba maalum hutumika ili kupunguza ukubwa wa mishipa ya damu. Dawa ya bawasiri sugu ni upasuaji.

Kinga ya Bawasiri

Kuhakikisha unapata choo kilaini husaidia kuzuia bawasiri na kupunguza kujirudia kwa dalili za bawasiri. Hii huwezekana kwa kula vyakula vyenye nyuzinyuzi (fiber),kunywa maji ya kutosha, kuwa na uzito unaofaa, kuepuka kukaa kwa muda mrefu, kuepuka kujikamua wakati wa haja kubwa na kuepuka kubeba vitu vizito mara kwa mara. 3

Hitimisho

Bawasiri ni hali inayoweza kukera lakini mara nyingi hazina madhara mabaya kwa afya ya binadamu. Ugonjwa huu unaweza kuisha wenyewe ndani ya wiki. Bawasiri mara nyingi hujirudia, na hali huzidi kuwa mbaya kadiri muda unavyosonga mbele. Bawasiri ni tatizo la kawaida ambalo linaweza kuathiri watu wengi wakati fulani maishani mwao. Kwa bahati nzuri, kuna hatua ambazo mtu anaweza kuchukua kuboresha hali hii au kuzuia kujirudia. Kwa mfano, kuhakikisha ulaji wa chakula chenye ufumwele (fiber) mwingi na kunywa maji ya kutosha kunaweza kusaidia kuzuia tatizo la bawasiri.

Ili kupunguza dalili za bawasiri, unaweza kujaribu matibabu ya nyumbani kama vile kujikanda kwa barafu ili kupunguza uvimbe au kutumia dawa za kupunguza maumivu. Hata hivyo, ni muhimu kushauriana na daktari ikiwa dalili zinazidi kuwa mbaya au nafuu haijapatiakana baada ya muda mfupi ili kupata ushauri na matibabu sahihi.

Maswali Yanayoulizwa Mara kwa Mara (FAQs)

S: Je, ni yapi madhara ya bawasiri kwa mwanamke?
J: Madhara ya bawasiri kwa mwanamke yanaweza kuwa ya kukera na kuharibu ustawi wake wa kila siku. Wanawake wanaweza kukabiliwa na maumivu makali, kuvuja damu wakati wa kujisaidia haja kubwa, na hata kuhisi aibu au unyonge kwa sababu ya hali hii. Bawasiri inaweza kuathiri pia shughuli za kazi na kuleta changamoto za kijamii na kiakili. Ni muhimu kwa wanawake wanaokabiliwa na bawasiri kutafuta ushauri wa matibabu ili kupata suluhisho sahihi na kuboresha hali yao ya afya na ustawi.

S: Je, bawasiri husababishwa na nini?
J: Bawasiri hutokana na sababu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na matatizo ya choo kigumu au kuhara, shinikizo la ziada tumboni wakati wa ujauzito, kuketi kwa muda mrefu, kuwa na uzito kupita kiasi, na mabadiliko ya homoni wakati wa ujauzito. Matatizo haya husababisha kuziba kwa mishipa ya damu kwenye njia ya haja kubwa, na hivyo kusababisha bawasiri. Kudumisha mtindo wa maisha wenye manufaa kiafya ni muhimu katika kuzuia tatizo hili au kupunguza hatari ya kukabiliwa nalo.

S: Je, dawa ya bawasiri sugu ni ipi?
J: Dawa ya bawasiri sugu inaweza kutofautiana kulingana na hali ya mtu binafsi na ukali wa bawasiri husika. Katika matukio ya bawasiri sugu, mtaalamu wa afya anaweza kupendekeza matibabu mbalimbali kama vile matumizi ya mafuta au vidonge vya kupunguza maumivu, dawa za kupaka ili kupunguza uvimbe, na mabadiliko ya mtindo wa maisha kama vile lishe bora yenye ufumwele mwingi na kunywa maji ya kutosha. Katika hali mbaya zaidi, upasuaji unaweza kuhitajika kutibu bawasiri sugu. Hivyo basi, ni muhimu kushauriana na mtaalamu wa afya ili kupata matibabu sahihi.