1. Ada
  2. Magonjwa
  3. Maambukizi ya kaswende (syphilis)

Maambukizi ya kaswende (syphilis)

Imeandikwa na Timu ya Ada ya Maarifa ya Kitiba

Imesasishwa tarehe

Kaswende ni nini?

Kaswende, inayofahamika kama “syphilis” kwa Kiingereza, ni ugonjwa wa maambukizi ya bakteria kwa njia ya kujamiiana (STD). Kaswende inayotambuliwa katika hatua za awali hujulikana kama hatua ya kwanza ya kaswende (primary syphilis).

Dalili za awali ni pamoja na vidonda vidogo kwenye sehemu za siri na tezi za limfu kuvimba. Ugonjwa huu huathiri sehemu tofauti za mwili, kwa hiyo dalili za baadaye hutofautiana kutoka mtu mmoja hadi mwingine. Kutumia kinga wakati wa kujamiiana huweza kupunguza uwezo wa kupata kaswende.

Antibiotiki hutumiwa kutibu maambukizi haya. Kwa matibabu ya mapema na sahihi, watu wengi hupona vizuri.

Visababishi vya ugonjwa wa kaswende

Ugonjwa wa kaswende unasababishwa na maambukizi ya bakteria aina ya Treponema pallidum. Kama maambukizi hayajatambuliwa na kutibiwa, maambukizi ya kaswende husababisha vipindi vya dalili, na hivi hujulikana kama kaswende ya hatua ya kwanza, ya pili na ya tatu. Inaweza kuchukua miaka kadhaa kutoka hatua ya kwanza hadi ya tatu. Vijana wenye umri kati ya miaka 15 na 24 huathirika zaidi.

Dalili za kaswende

Dalili za kaswende ambazo hujitokeza awali ni pamoja na:

  • Kidonda kwenye sehemu za siri, mdomo au makalio
  • Kuvimba kwa tezi za limfu kwenye kinena

Dalili hizi kawaida huisha ndani ya wiki kadhaa na mara nyingine dalili hizi zinaweza zisitambulike.

Ugonjwa unavyoendelea, mtu aliyeathirika anaweza kupata dalili nyingine, zikiwemo:

  • Vipele
  • Homa
  • Maumivu ya viungo
  • Kupoteza nywele
  • Viuvimbe vidogo kwenye sehemu za siri
  • Maumivu ya misuli

Hatua za baadaye za ugonjwa wa kaswende huendelea polepole ndani ya miaka, na huathiri moyo, ubongo na sehemu nyingine za mwili. Hii inaweza kusababisha dalili tofauti, kama vile:

  • Kuishiwa pumzi
  • Kuchanganyikiwa
  • Kusahau
  • Kupoteza uratibu
  • Uharibifu wa neva na vinginevyo

Utambuzi wa kaswende

Utambuzi hufanywa kulingana na dalili, uchunguzi wa kimwili na vipimo vya damu kwa uwepo wa protini dhidi ya kaswende. Utambulizi mara nyingi hufanywa wakati wa uchunguzi wa kawaida, kwa sababu kaswende inaweza isisababishe dalili zozote, au dalili zisizo za kawaida.

Kama kuna kidonda, sampuli ya majimaji kutoka kwenye kidonda huweza pia kuchunguzwa kwa uwepo wa bakteria. Hamna kipimo kimoja cha kutambua magonjwa yote ya zinaa. Tafadhali ongea na mtaalamu wa afya kwa taarifa zaidi.

Matibabu (Treatment of syphilis)

Kaswende hutibiwa kwa antibiotiki. Vipimo hufanyika baada ya matibabu ya kaswende ili kuhakikisha maambukizi yametibiwa kikamilifu. Penisilini ya Benzathine ndiyo chaguo la kwanza la tiba kwa hatua zote za kaswende. Machaguo mengine, haswa ikiwa mtu aliyeathirika ana mzio wa penisilini, ni doxycycline na ceftriaxone. Penisilini ya Benzathine kwa kawaida ni sindano inayochomwa kwenye misuli, wakati doxycycline na ceftriaxone kwa kawaida huchomwa kwenye mishipa ya damu au misuli. Dawa zote tatu hutolewa kwa dozi kubwa, kwa siku moja au siku kadhaa mfululizo. Penisilini ya Benzathine inaweza kutolewa katika dozi tofauti, kulingana na hatua iliyofikia kaswende inayotibiwa.

Mara nyingi si lazima kwa mtu anayepata matibabu ya aina hii kulazwa hospitalini. Lakini, ukubwa wa dozi na njia inayotumika kuitoa kwa kawaida husababisha matibabu kufanyika chini ya uangalizi wa daktari au muuguzi. Uangalizi huu pia huboresha uwezekano wa mtu aliyeathirika kukamilisha matibabu, kwani kupata dozi moja iliyotolewa na daktari humaanisha kuwa hakuna uwezekano wa mtu aliyeathirika kukosa kutumia dawa anaporudi nyumbani.

Baada ya matibabu, watu hupata nafuu haraka. Hata hivyo, hali inayojulikana kama muitikio wa Jarisch-Herxheimer inaweza kujitokeza muda mfupi baada ya kutumia antibiotiki, kwani vijidudu vinavyokufa vya Treponema pallidum hutoa sumu kwenye mkondo wa damu. Hali hii huwa ni ya muda mfupi na kwa kawaida huwa siyo hatarishi. Dalili zake ni pamoja na:

Ikiwa hali hii itatokea, antibiotiki hazitositishwa, lakini kotikosteroidi kama vile prednisone au cortisone inaweza kupendekezwa kama sehemu ya matibabu.

Kinga

Kutumia kinga wakati wa kujamiiana huweza kuzuia maambukizi mapya ya kaswende. Wanawake wajawazito wanapaswa kuchunguzwa (kupimwa bila kuwa na dalili) ili kuzuia kusambaza bakteria hawa kwa mtoto.

Ubashiri

Kwa utambuzi na matibabu ya mapema, watu wengi hupona vizuri na hawana matatizo ya kudumu. Kaswende isiyo tibiwa inaweza kusambaa katika sehemu nyingine za mwili, na kusababisha uharibifu wa mishipa ya damu, ubongo na neva.

Ikiwa itatibiwa ipasavyo kwa antibiotiki, hatua ya kwanza na ya pili ya kaswende huwa na matokeo mazuri sana. Hata hivyo, kwakuwa hatua ya mwisho ya kaswende (tertiary syphilis) kwa kawaida hutokea baada ya miaka mingi ya maambukizi ya awali, kwa ujumla matokeo ya kaswende hutofautiana. Hatua ya mwisho ya kaswende ambayo haijatibiwa inaweza kusababisha kifo, haswa ikiwa imeathiri moyo na mishipa ya damu. Lakini, watu wanaopata uvimbe kwenye hatua ya mwisho ya kaswende (gummatous tertiary syphilis) mara nyingi hupata nafuu baada ya matibabu.

Watoto wachanga waliozaliwa na maambukizi ya kaswende huwa na matokeo tofauti, lakini wanaweza kufa.

Watu walioathirika na kaswende ya mfumo wa neva (neurosyphilis) huwa na matokeo tofauti baada ya matibabu. Watu walio na kaswende ya mfumo wa neva isiyo na dalili na kaswende ya mfumo wa neva inayoathiri tishu inayozunguka ubongo na uti wa mgongo (meningeal neurosyphilis) kwa kawaida hupona. Watu walio na kaswende ya tishu na mishipa ya damu ya ubongo na uti wa mgongo (meningovascular) wanaweza kupata nafuu. Lakini, haswa ikiwa walipatwa na kiharusi, mara chache hurudi katika afya ya kawaida.

Kwa ujumla athari za kwenye ubongo na uti wa mgongo zinazotokana na hatua ya mwisho ya kaswende hudumu maishani: ingawa mtu aliyeathirika anaweza kupata nafuu, hawezi kurudi katika hali yake ya kawaida kiutendaji kutokana na athari ambazo zimeshatokea. Hivyo basi, kadiri ugonjwa unavyotambuliwa na kutibiwa mapema, ndivyo matokeo ya matibabu yanavyokuwa mazuri zaidi.

Maswali Yanayoulizwa Mara kwa Mara kuhusu Kaswende (FAQs)

S: Je, kaswende inaambukiza?
J: Ndiyo. Kaswende inaweza kuambukizwa kutoka mtu mmoja hadi mwingine. Watu wengi hupata maambukizi haya kwa kujamiiana na mtu aliyeambukizwa, lakini pia kuna uwezekano kwa akina mama wenye kaswende kuwaambukiza watoto wao wakati wa ujauzito. Katika matukio machache, watu wanaotumia vitu ambavyo vimetumiwa na wengine kama vile sindano wanaweza kupata kaswende ikiwa sindano imetumiwa na mtu aliye na kaswende.

S: Nani anapaswa kupimwa kaswende (syphilis test)?
J: Wale wanaopaswa kupimwa kaswende ni pamoja na:

  • Mtu yeyote asiye na dalili ambaye ana hofu kwamba anaweza kuwa ameambukizwa kaswende na mtu aliye jamiiana naye au mpenzi wake
  • Mtu yeyote anayeonyesha dalili zozote za hatua yoyote ya kaswende
  • Wanawake wote wajawazito au wanawake wanaopanga kuwa wajawazito
  • Mtu yeyote ambaye hivi karibuni ameshiriki tendo la kujamiiana bila kinga na mpenzi mpya ambaye hali yake ya maambukizi ya magonjwa ya kujamiiana (STI) haifahamu
  • Mtu yeyote ambaye hivi karibuni amefanya tendo la kujamiiana bila kinga na wapenzi wengi
  • Mtu yeyote ambaye ana magonjwa mengine yanayoambukizwa kwa njia ya kujamiiana, kama vile klamidia au kisonono, au ambaye mpenzi wake ametambulika kuwa ana STI
  • Mtu yeyote ambaye ana Virusi vya Ukimwi (VVU)
  • Wanaume wanaojamiiana na wanaume wenzao
  • Mtu yeyote ambaye alikwishawai kuambukizwa kaswende

S: Nifanye nini ikiwa nadhani nina maambukizi ya kaswende?
J: Yeyote anayeshuku huenda akawa na maambukizi ya kaswende anapaswa kwenda kwa daktari, kliniki au kliniki maalum inayoshughulika na afya ya viungo vya uzazi na kuomba kupimwa kaswende.

S: Je, watu ambao hawaonyeshi dalili lakini wanajishuku huenda wameambukizwa kaswende wanapaswa kuomba kupimwa kaswende?
J: Ndiyo. Inawezekana kwa kaswende kutokuwa na dalili zozote. Ikiwa unahisi umeambukizwa kaswende na mpenzi wako, lakini hauonyeshi dalili, unapaswa kuomba kupimwa. Ni muhimu zaidi kufanyiwa kipimo cha kaswende ikiwa unatarajia kuwa mjamzito, umefanya tendo la kujamiiana bila kinga, au una wapenzi wengi.

S: Je, watu wanaojamiiana bila kinga wako katika hatari ya kuambukizwa kaswende?
J: Ndiyo. Kaswende huambukizwa kwa njia ya kujamiiana, kama vile kujamiiana kunakohusisha mdomo (oral sex), kujamiiana kinyume na maumbile na kujamiiana ukeni, na vile vile kupitia migusano mingine ya ukeni na uumeni ikiwemo pia matumizi ya midoli wakati wa kujamiiana. Kaswende huambukiza wakati wa kujamiiana kwa kugusana moja kwa moja na kidonda kitokanacho na maambukizi (chancre). Kujikinga na uwezekano wa kugusa kidonda chenye maambukizi, kwa mfano kwa kutumia kondomu au kutumia kinga ya kinywani (dental dam), hupunguza hatari ya kuambukizwa kaswende.

S: Je, mtu anaweza kuambukizwa kaswende kwa kutoa huduma ya kwanza kwa mtu aliye na kaswende?
J: Kaswende ni ugonjwa unaobebwa na damu, na inawezekana kwamba kugusa damu ya mtu aliye na kaswende, kama inavyoweza kutokea wakati wa kutoa huduma ya kwanza, kunaweza kusambaza maambukizi. Hata hivyo, kwa watoa huduma ya kwanza na wataalamu wa matibabu ya dharura, hatari kubwa ipo kwenye uwezekano wa kupata jeraha litokanalo na sindano yenye maambukizi ya kaswende.

S: Je, mtu anaweza kupata kaswende kwa kutumia midoli na mtu mwingine wakati wa kujamiiana?
J: Ndiyo, ikiwa mmoja wa wapenzi katika tendo la kujamiiana ana kaswende, na wanatumia midoli katika tendo husika. Hatari ya uwezekano wa kuambukizana kaswende inaweza kupungua kwa kufanya yafuatayo:Kuvalisha kondomu kwenye midoli, na kila mshiriki kutumia kondomu mpya.Kusafisha midoli vizuri wakati wa matumizi, kwa kutumia sabuni na maji au kemikali maalum ya kusafishia midoli.Tumia aina sahihi ya kilainishi, kwani kutumia aina isiyo sahihi itasababisha uharibifu wa eneo la mdoli, na kufanya kuwa vigumu zaidi kusafisha.


Washirikishe wengine kwenye makala hii: