1. Ada
  2. Magonjwa
  3. Ugonjwa wa PID

Ugonjwa wa PID

Imeandikwa na Timu ya Ada ya Maarifa ya Kitiba

Imesasishwa tarehe

Maambukizi ya via vya uzazi vya mwanamke ni nini?

Maambukizi ya via vya uzazi vya mwanamke au ugonjwa wa PID (pelvic inflammatory disease) ni maambukizi ya bakteria kwenye shingo ya uzazi, mirija ya fallopio, ovari na tumbo la uzazi (uterasi).

Sababu kuu ya ugonjwa huu kutokea ni maambukizi yanayosambazwa kwa kujamiiana (STI). Ugonjwa huu unaweza kuwaathiri wanawake wenye umri wowote, lakini wale wenye umri kati ya maika 15 na 24 huathirika zaidi.

Dalili huweza kujumuisha: maumivu ya nyonga au tumbo, maumivu wakati wa kujamiiana, na uchafu usio wa kawaida kutoka ukeni pamoja na homa. PID hutibiwa kwa antibiotiki, na utambuzi na matibabu ya mapema ni muhimu katika kuzuia madhara ya kupata makovu na utasa. 1

Vihatarishi vya ugonjwa wa PID

Maambukizi ya via vya uzazi vya mwanamke ni semi ya kitabibu inayoelezea maambukizi ya shingo ya uzazi, tumbo la uzazi na mirija ya fallopio. Kwa kawaida maambukizi haya husababishwa na bakteria.

Ingawa mara nyingi ni maamkubizi yanayosambazwa kwa njia ya kujamiiana (STI), kama vile klamidia au kisonono, wakati mwingine maambukizi haya huweza kusababishwa na bakteria wengine. PID inaweza kuwaathiri wanawake wenye umri wowote, lakini wale wenye umri kati ya miaka 15 and 24 huathirika zaidi.

Dalili za PID

Dalili huweza kujumuisha: 1 2

  • Maumivu kwenye nyonga na tumbo
  • Maumivu wakati wa kujamiiana
  • Kutokwa damu nyingi wakati wa hedhi
  • Kutokwa na majimaji yasiyo ya kawaida ukeni

Baadhi ya watu huweza kupata homa, kichefuchefu, kutapika au maumivu wakati wa kujisaidia.

Utambuzi

Utambuzi mara nyingi huweza kufanywa kulingana na dalili na uchunguzi wa sehemu za siri. Wakati wa uchunguzi, sampuli za majimaji au usaha huchukuliwa ili kutambua bakteria anayesababisha maambukizi.

Matibabu (PID treatment)

Maambukizi ya via vya uzazi vya mwanamke hutibiwa kwa antibiotiki. Na tiba ya PID hutofautiana kulingana na ukali wa maambukizi. Ikiwa maambukiz ni makali, inaweza kuhitajika kupewa antibiotiki kupitia mishipa ya damu. Ikiwa maambukizi husababisha usaha kukusanyika au makovu kwenye mirija ya fallopio, basi upasuaji huweza kuhitajika ingawa hii ni nadra sana. 3

Ubashiri

Watu wengi hupona vizuri baada ya matibabu na maambukizi hayasababishi matatizo ya muda mrefu. Hata hivyo, ikiwa maambukizi hayatatibiwa, au ikiwa mtu anayapata maambukizi haya tena baada ya kutibiwa, basi kuna uwezekano mkubwa wa kupata madhara zaidi. Haya huweza kujumuisha makovu kwenye tumbo la uzazi na mirija ya fallopio, ugumu wa kupata mimba, mimba kutungwa nje ya tumbo la uzazi, na maumivu ya muda mrefu ya nyonga.

Kinga

Njia muhimu ya kuzuia maambukizi ya via vya uzazi vya mwanamke ni kutumia kondomu wakati wa kujamiiana. Kondomu ni njia bora ya kuzuia kupata maambukizi yanayosambazwa kwa njia ya kujamiiana (STIs). Watu waliotambuliwa kuwa na STI wanapaswa kuwataarifu wapenzi wao ili wapimwe na kutibiwa pia.